Na Mwandishi Wetu
HALMASHAURI ya Wilaya
ya Mbarali mkoani Mbeya imesema imejizatiti kuja na timu bora kwenye Mashindano
ya Shirikisho la Michezo ya Serikali za
Mitaa nchini(Shimisemita) yanayotarajiwa kufanyika mkoani Mbeya Septemba mwaka
huu.
Hayo yamebainishwa na
Mkuu wa Idara ya Michezo, Sanaa na Utamaduni, Mariam Mnozya alipokuwa akifunga
bonanza la Michezo lililowakutanisha watumishi wa halmashauri hiyo huku pia
timu za Tanesco na Magereza zikishiriki kama waalikwa.
Watumishi walioshiriki
bonanza hilo la michezo lililofanyika kwenye viwanja vya Shule ya Sekondari
Rujewa ni kutoka Kata tano za Tarafa ya Rujewa ambazo ni Rujewa , Lugelele
,Imalilo songwe , Ubaruku na Mawindi.
Katika bonanza hilo,
Mnozya amesisitiza umuhimu wa watumishi kuzingatia mazoezi ya mara kwa mara ili
kufanya miili yao kuwa sawa na tayari kwa mashindano ya Shimisemita.
Amesema pamoja na
kuimarisha miili kiafya ni muhimu watumishi wa halmashauri hiyo kama ilivyo kwa
wenzao wa halmashauri zote za Mkoa wa Mbeya kuzingatia mazoezi ili kuleta
ushindani kwenye mashindano ya Shimisemita mwaka huu kwakuwa ndiyo watakuwa
wenyeji.
"Kama tunavyojua
sisi ni wachezaji lazima tufanye mazoezi ili kuhakikisha tunakuwa na timu bora zitakazoweza kushindana na kutoa
changamoto kwa wapinzani.Mazoezi haya yasiishie hapa tuendelee kufanya mara kwa
mara maana mashindano ya mwaka huu sisi kama Mkoa wa Mbeya ni wenyeji wa hivyo
hatuwezi kukubali kutoka kwa aibu. " amesisitiza Mnozya
Bonanza hilo lenye
lengo la kuibua vipaji vya wachezaji watakaounda Timu ya Halmashauri ya Wilaya
ya Mbarali itakayokwenda kushiriki michuano ya Shimisemita mwaka huu
lilihusisha michezo mbalimbali ikiwemo mpira wa miguu, kikapu ,mikono, wavu, pete,
bao na karata.








No comments:
Post a Comment