Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Sunday, April 12, 2026

DC NYAKIA ASISITIZA MICHEZO KWA AFYA NA UCHUMI

 




Na Mwandishi Wetu

MKUU wa Wilaya ya Sumbawanga, Nyakia Ally Chirukile amesisitiza kuwa michezo ni muhimu katika kuimarisha Afya na Uchumi wa wananchi hivyo ni muhimu kila mwanajamii wakiwemo watumishi kuizingatia.

 

Chirukile ameyasema hayo wakati akifungua Bonanza la Michezo la watumishi lililofanyika katika Uwanja wa Kumbukumbu wa Nelson Mandela uliopo katika Manispaa ya Sumbawanga Mkoani Rukwa.

 

Chirukile amesema kuwa michezo sio tu hufungua fursa za kiuchumi, bali pia huimarisha undugu na mshikamano baina ya jamii.

 

"Michezo ni afya, michezo hufungua fursa za uchumi na kuimarisha undugu baina ya Jamii hivyo mabonanza kama haya yafanyike mara kwa mara ili kuchechemua maendeleo endelevu baina yetu," amesema Chirukile.

 

Aidha Mkuu huyo wa Wilaya amesisitiza kuwa Serikali inaunga mkono michezo katika jamii na kuwahamasisha wananchi kushiriki katika shughuli za michezo ili kuboresha afya zao na kuchangia maendeleo ya uchumi wa Taifa.

 

Bonanza hilo limehusisha timu kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga, Wilaya ya Mbozi na Wilaya ya Nkasi, zikishindana katika michezo mbalimbali kama vile mpira wa miguu, mpira wa pete, mpira wa mikono, mpira wa wavu, bao, drafti, na karata.

MBARALI WAJIPANGA USHINDANI SHIMISEMITA 2026

 









Na Mwandishi Wetu

 

HALMASHAURI ya Wilaya ya Mbarali mkoani Mbeya imesema imejizatiti kuja na timu bora kwenye Mashindano  ya Shirikisho la Michezo ya Serikali za Mitaa nchini(Shimisemita) yanayotarajiwa kufanyika mkoani Mbeya Septemba mwaka huu.

 

Hayo yamebainishwa na Mkuu wa Idara ya Michezo, Sanaa na Utamaduni, Mariam Mnozya alipokuwa akifunga bonanza la Michezo lililowakutanisha watumishi wa halmashauri hiyo huku pia timu za Tanesco na Magereza zikishiriki kama waalikwa.

 

Watumishi walioshiriki bonanza hilo la michezo lililofanyika kwenye viwanja vya Shule ya Sekondari Rujewa ni kutoka Kata tano za Tarafa ya Rujewa ambazo ni Rujewa , Lugelele ,Imalilo songwe , Ubaruku na Mawindi.

 

Katika bonanza hilo, Mnozya amesisitiza umuhimu wa watumishi  kuzingatia mazoezi ya mara kwa mara ili kufanya miili yao kuwa sawa na tayari kwa mashindano ya Shimisemita.

 

Amesema pamoja na kuimarisha miili kiafya ni muhimu watumishi wa halmashauri hiyo kama ilivyo kwa wenzao wa halmashauri zote za Mkoa wa Mbeya kuzingatia mazoezi ili kuleta ushindani kwenye mashindano ya Shimisemita mwaka huu kwakuwa ndiyo watakuwa wenyeji.

 

"Kama tunavyojua sisi ni wachezaji lazima tufanye mazoezi ili kuhakikisha tunakuwa  na timu bora zitakazoweza kushindana na kutoa changamoto kwa wapinzani.Mazoezi haya yasiishie hapa tuendelee kufanya mara kwa mara maana mashindano ya mwaka huu sisi kama Mkoa wa Mbeya ni wenyeji wa hivyo hatuwezi kukubali kutoka kwa aibu. "  amesisitiza Mnozya

 

Bonanza hilo lenye lengo la kuibua vipaji vya wachezaji watakaounda Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali itakayokwenda kushiriki michuano ya Shimisemita mwaka huu lilihusisha michezo mbalimbali ikiwemo mpira wa miguu, kikapu ,mikono, wavu, pete, bao na karata.

Friday, April 3, 2026

DKT TULIA AKABIDHI NYUMBA KWA MHITAJI KATA YA ITEZI

 




Na Joachim Nyambo,Mbeya 

RAIS wa Umoja wa Mabunge Duniani(IPU) ambaye pia ni Spika mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Uyole Dkt Tulia Ackson amekabidhi nyumba ya 25 kwa Elizabeth Jimmy (72) mkazi wa Mtaa wa Mwasote Kata ya Itezi Jijini Mbeya.

 

Kabla ya kukabidhi nyumba Dkt Tulia Ackson amepokea bendera ya upendo kutoka kwa kiongozi wa mbio za bendera Lugano Mwangosi ambapo kaya 160 zenye watu zaidi ya watu 1000 zilinufaika kupitia mbio hizo kwa kupewa chakula.

 

Mwangosi amesema katika mbio hizo pia wamebaini changamoto mbalimbali zinazoikabili wahitaji wakiwemo watu wenye ulemavu wanaohitaji Viti mwendo na miguuni bandia.

 

Diwani wa Kata ya Itezi, James Kapolesya amekabidhi kitanda na godoro kwa nia ya kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Mbunge.

Katika hotuba yako Dkt Tulia Ackson amesema Taasisi ya Tulia Trust amesema Taasisi yake hujenga nyumba kutokana na uhitaji kama kuna mtu anaona nyumba ni ndogo na atatamani kuishi hapo alete hitaji lake ili vyumba viongezwe.

 

Dk Tulia Ackson amesema wahitaji ni wengi hivyo tupendane katika jamii kwa kusaidia watu wenye uhitaji hata kwa kuwasaidia chakula.

 

Amesema hoja za wakimbiza bendera amezipokea wakiwemo wa matibabu na watu wenye ulemavu wanaohitaji Viti mwendo watapatiwa baada ya sikukuu.

 

Amesema mpango wa mwaka huu ni kujenga nyumba moja kila Kata hivyo zitajengwa nyumba 13 na ametumia fursa hiyo kuwashukuru wadau wote waliomuunga mkono kwa kutoa vitu mbalimbali vikiwemo vyakula, nguo na mablanket.

 

Amehitimisha kuwa shughuli za kuisadia jamii ni endelevu zikiwemo kusomesha, matibabu na ujenzi wa nyumba.

 

Spika mstaafu wa Uswisi Maya Riniker kupitia Chama cha FDP amempongeza Dkt Tulia Ackson kwa namna anavyoisaidia jamii kwa kutoa misaada mbalimbali na amefurahi kwa namna wananchi wanavyozikubali kazi zake.

 

Chifu George Lyoto kwa niaba ya Viongozi wa mila amepongeza juhudi zinazofanywa na Mbunge pia amesema wapuuzwe wanaobeza kazi zinazofanywa na Mbunge.

 

Katibu Mwenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM)Kata ya Itezi Jijini Mbeya, Raphael Mwaitege amelaani vikali la watu wanaobeza zoezi la ujenzi wa nyumba za wahitaji linalofanywa na Spika mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Uyole Dkt Tulia Ackson kuwa nyumba zinazojengwa kuwa ni ndogo wakati wao hawajawahi kutoa hata misumari.

 

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi CCM Kata ya Itezi Gervas Lameck Lonje amesema njia pekee ya kushikamana na Dkt Tulia Ackson ni kuunga mkono juhudi zinazofanywa za kuwasaidia wahitaji.


Aidha Mwenyekiti wa Jumuya ya Wazazi Wilaya ya Mbeya Mjini, Emmanuel Mwalupindi ambaye alimwakilisha Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mbeya Mjini amesema kwa sasa hakuna muda wa kusikiliza maneno bali ni wakati wa kufanya kazi kwa vitendo kwani kila mmoja akisaidia wahitaji atakuwa anapata thawabu mbele za Mungu.

 

Kwa upande wake Elizabeth Jimmy amemshukuru sana Dk Tulia Ackson kwa kumjengea nyumba ya kudumu kwani imemuondokea kadhia ya kupanga iliyokuwa inamkabili.

Monday, March 30, 2026

AFISA ZIMAMOTO MBEYA AWAPA TABASAMU WAHITAJI

 










Na Joachim Nyambo,Mbeya

Afisa Habari Msaidizi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Mbeya Sajenti Esther Dismas Kinyaga ambaye pia ni Makamu Mkuu wa Idara ya Uhitaji Maafa na Makundi Maalum Taifa (SMAUJATA), ameacha alama ya matumaini na faraja baada ya kushiriki kama mgeni rasmi katika ziara ya kutembelea kituo cha kulea watu wenye ulemavu kilichopo Iyunga, Jijini Mbeya.

Ziara hiyo imeandaliwa na kundi la Mbeya Generation, ikiwa na lengo la kuwafariji na kuwatia moyo watoto wenye ulemavu wanaolelewa katika kituo hicho, pamoja na kuihamasisha jamii juu ya umuhimu wa kuwajali na kuwaunga mkono.
Akizungumza katika tukio hilo, Sajenti Kinyaga alitoa mafunzo ya kuwaimarisha kisaikolojia kwa watoto hao na walezi wao, akisisitiza umuhimu wa kujithamini, kuwa na matumaini na kujiamini licha ya changamoto zinazowakabili katika maisha yao ya kila siku.
“Ulemavu sio mwisho wa maisha, kila mmoja ana thamani yake katika jamii hivyo ni muhimu kuendelea kupambana na kutumia fursa zilizopo kujijenga na kutimiza ndoto zenu,” alisisitiza Kinyaga.
Aidha aliwataka wananchi na wadau mbalimbali kuendelea kuwaunga mkono watu wenye ulemavu kwa vitendo, ikiwemo kuwapatia mahitaji muhimu na kuhakikisha wanapata fursa sawa katika nyanja zote za maisha.
Katika kuonesha upendo na mshikamano, Sajenti Kinyaga alikabidhi zawadi mbalimbali kwa watoto hao hatua iliyowaletea furaha na tabasamu huku ikionyesha umuhimu wa kugusana na jamii zinazohitaji msaada.
Tukio hilo limeacha kumbukumbu ya kipekee ya upendo, mshikamano na matumaini mapya kwa watoto hao pamoja na walezi wao, likiwa ni chachu ya kuendelea kuhamasisha jamii kujenga moyo wa kujali na kusaidiana.

MWENYEKITI JUMUIYA YA WAZAZI CCM MBEYA MJINI ATOA JEZI KWA WASHINDI LIGI YA WANAWAKE

 





Na Joachim Nyambo,Mbeya

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Mbeya Mjini, Emmanuel Mwalupindi amekabidhi zawadi ya jezi kwa timu ya Icons Queens iliyofanya vizuri na kuibuka washindi katika ligi ya wanawake mkoani Mbeya, ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha na kuendeleza michezo kwa wanawake.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano hayo, Mwalupindi amesema kuwa michezo ni nyenzo muhimu ya kuwawezesha wanawake kijamii na kiuchumi, huku akisisitiza umuhimu wa kuendelea kuwekeza katika sekta hiyo ili kukuza vipaji vya vijana wa kike.

Ameongeza kuwa Jumuiya ya Wazazi itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha wanawake wanapata fursa zaidi za kushiriki katika michezo na kuonesha uwezo wao, jambo litakalosaidia kuinua hadhi ya michezo ya wanawake katika ngazi ya mkoa na taifa kwa ujumla.

Kwa upande wao, baadhi ya wachezaji wa timu hiyo wameeleza kufurahishwa na zawadi hiyo, wakisema kuwa imewapa motisha ya kuendelea kufanya vizuri zaidi katika mashindano yajayo. Wameomba wadau wengine kujitokeza kusaidia maendeleo ya michezo ya wanawake ili kufikia mafanikio makubwa zaidi.

Ligi hiyo ya wanawake mkoani Mbeya imekuwa chachu ya kugundua na kukuza vipaji vya soka kwa wanawake, huku ikitoa fursa kwa timu mbalimbali kushiriki na kujenga ushindani wenye tija.

Friday, March 13, 2026

KAMATI YA BUNGE YA MAJI NA MAZINGIRA YATUA IRINGA






Sehemu ya wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Maji na Mazingira baada ya kuwasili mkoani Iringa

Na Mwandishi Wetu

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira ikiongozwa na Mwenyekiti wake Mhe. Jackson Kiswaga Machi 12, 2026 imewasili katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa kwa ajili ya ziara ya kutembelea Mradi wa Urejeshwaji Endelevu wa Mazingira na Hifadhi ya Bayoanuai Tanzania (SLR) unatekelezwa na Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa la Mazingira (UNEP) katika Halmashauri ya Iringa.

Wajumbe hao wameambatana na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Festo Dugange, Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Balozi Baraka Luvanda na watendaji kutoka Ofisi hiyo.

Akizungumza, Dkt. Dugange alisema mradi huo unawezesha wananchi kufanya shughuli za kiuchumi bila kuathiri mazingira.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Kheri James alipongeza Ofisi ya Makamu wa Rais kwa utekelezaji wa mradi huo na kusema unasaidia kulinda mazingira.

Mradi huo pia unatekelezwa katika Halmashauri za Wilaya za Wanging’ombe, Mbarali na Mbeya katika bonde la Ruaha Mkuu na halmashauri za Sumbawanga, Mpimbwe na Tanganyika katika Bonde la Ziwa Rukwa.

Thursday, May 15, 2025

HUYU HAPA MWAMUZI MCHEZO WA FAINALI KOMBE LA SHIRIKISHO


 Baada ya kuthibitishwa kwa uwanja wa mechi, Shirikisho la Soka Barani Afrika (CAF) limetangaza uteuzi rasmi wa waamuzi kwa fainali ya Kombe la Shirikisho la CAF.

CAF imemteua mwamuzi wa kimataifa kutoka Mauritania, Dahane Beida, kuwa mwamuzi wa kati katika mchezo wa marudiano wa fainali ya Kombe la Shirikisho la CAF kati ya Simba SC ya Tanzania na RS Berkane ya Morocco. Mchezo huo umepangwa kufanyika tarehe 25 Mei 2025 katika Uwanja wa Amaan Zanzibar.
Dahane Beida ni mwamuzi mwenye uzoefu mkubwa katika soka la Afrika. Miongoni mwa mechi kubwa alizowahi kuzisimamia ni fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) mwaka 2023 kati ya Ivory Coast na Nigeria. Pia, alisimamia mechi ya marudiano ya fainali ya Kombe la Shirikisho la CAF msimu wa 2022/23.
Fainali ya mwaka huu inatarajiwa kuwa ya kusisimua, kwani Simba SC itakuwa inacheza fainali yake ya kwanza ya Kombe la Shirikisho, huku RS Berkane wakitafuta taji lao la tatu katika mashindano haya, baada ya kulibeba mwaka 2020 na 2022.
Mchezo wa kwanza wa fainali hiyo utafanyika tarehe 17 Mei 2025 katika Uwanja wa Berkane Municipal, Morocco.

Saturday, April 19, 2025

MRATIBU MISS TANZANIA AFARIKI DUNIA

 


Mratibu wa zamani wa Miss Tanzania Hashim Lundega, amefariki dunia leo Jijini Dar es Salaam.

Lundenga ambaye ameugua kwa muda mrefu itakumbukwa ndio aliyesimamia kwa mafanikio makubwa Mashindano ya Urembo Tanzania na kuyapa umaarufu mashindano hayo.

Lundenga pia aliwahi kuhudumu kwenye Kamati ndani ya Klabu ya Yanga.

Thursday, April 17, 2025

SIMBA YALAMBA MKATABA MNONO

 


Mkataba Wa Simba Sports Club Na JayRutty ni wa Shilingi Bilioni 38 kwa miaka mitano.

Kuna gawiwo la 5.6 Bilioni kila mwaka na ongezeko la asilimia 10 kwa kila mwaka 

FAIDA ZA KIMKATABA.

1. Ujenzi wa Uwanja wa Bunju (Watu Elf10 hadi 12).

2. Gari la IRIZAR .

3. Media production.

4. Ujenzi wa Ofisi Mpya

5. Kukuza Vipaji ( pesa cash kutolewa)

6. Pre seasons sponsorship

7. Medica room

8. Simba Day ( pesa itatolewa cash m100)

9. Motisha kwa wachezaji ( M470 cash)

10. Jezi za brand kubwa dunia

YANGA TANGA,SIMBA MANYARA



SHIRIKISHO la Soka Tanzania(TFF) limepanga mchezo wa nusu fainali ya kwanza ya CRDB Federation Cup kati ya bingwa mtetezi Yanga SC dhidi ya JKT Tanzania kufanyika katika dimba la CCM Mkwakwani Jijini Tanga.

Nusu fainali nyingine imepangwa kuchezwa katika uwanja wa Tanzanite Kwaraa Manyara ikiwakutanisha Simba SC dhidi ya Singida Black Stars. 

Michezo hiyo ya kuwatafuta wanafainali wa Federation Cup 2024-2025 imepangwa kufanyika kati ya Mei 16-18, 2025.

Tuesday, April 8, 2025

ARSENAL KUIVAA REAL MADRID USIKU WA LEO UEFA

 

Klabu ya Arsenal ya Uingereza, usiku wa leo inawakaribisha mabingwa mara 15 wa Ulaya, Real Madrid katika mechi ya kwanza ya hatua ya Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya (UEFA), katika mchezo utakaofanyika kwenye uwanja wa Emirates, jijini London.

Timu hizo zilikutana kwa mara ya mwisho kwenye msimu wa UEFA 2005/06, ambapo ‘The Gunners’ ilisonga mbele kuelekea hatua ya robo fainali kwa ushindi wa wa 1-0 dhidi ya Real Madrid.
Je, Arsenal itafanya maajabu leo mbele ya mabingwa hao wa kihistoria wa Ulaya?