Na Mwandishi Wetu,Mbarali
MSISIMKO wa Mashindano
ya Umoja wa Michezo na Taaluma Shule za Msingi Tanzania (UMITASHUMTA) kwa ngazi
ya Mkoa wa Mbeya yametamatika kwa wanafunzi takribani 120 kutoka Shule za
Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali kuibuka kidedea kwa kuwa washindi wa kwanza
mchezo wa mpira wa kikapu, washindi wa pili riadha na washindi nafasi ya tatu
michezo ya mpira wa miguu, mpira wa wavu na mpira wa pete hatua iliyopelekea
kuibuka na jumla ya vikombe vitano na vyeti vitatu
Mkurugenzi Mtendaji wa
Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali, Raymond Mweli amewapokea wanafunzi hao
ofisini kwake leo Juni 02, 2026 na kuwapongeza kwa ushindi huo huku akiwaahidi
kushirikiana na walimu, walezi na wazazi wao katika kuwaendeleza kitaaluma na
michezo pia.
“Nilipokuwa nawaaga
niliwasihi mkafanye vizuri na ninawapongeza hamjatuangusha, tutaendelea kulea
vipaji vyenu kwa kushirikiana na walimu, walezi na wazazi wenu na tutatumia
mashindano mbalimbali kuwaendelea kimichezo na kuitangaza Halmashauri yetu. Ni
muhimu sana mkasome kwa bidii na muwe na maadili mema kwa ajili ya maisha yenu
ya sasa na baadae na mtambue Taifa linawategemea”, amesema Mweli.
Aidha katika jumla ya wanafunzi 120 waliowakilisha Wilaya ya
Mbarali katika michezo hiyo, wanafunzi 15 wanaotokana na michezo mbalimbali
wamebaki kwenye kambi ya Mkoa wa Mbeya kwa ajili ya maandalizi ya kuuwakilisha
Mkoa katika ngazi ya michezo hiyo Kitaifa inayotarajiwa kuanza kufanyika Juni
06 mwaka huu Mkoani Iringa.
Kwa upande wake Kaimu
Afisa Michezo wa Wilaya ya Mbarali, Bi. Mariam Mnozya ametoa shukrani kwa
uongozi wa Halmashauri hiyo kwa kuwa nao bega kwa bega katika kila hatua
kuanzia hatua za awali za maandalizi ya mashindano hayo ambapo amesema utayari
wa uongozi huo imekuwa moja ya chachu ya mafanikio ya ushindi ambao
umepatikana.






No comments:
Post a Comment