Karibu katika blogu hii,kuwa mmoja wa wale wanaochangia na kujivunia mafanikio yake. Tunakualika kwa mikono miwili wasiliana nasi kwa simu 0756409597 au nyambojoachim@gmail.com

Sunday, July 28, 2024

MILIONI 10 KUKARABATI UWANJA WA SOKOINE




Na Lyamba Lya Mfipa

SHILINGI milioni kumi zinatarajiwa kutumika kwaajili ya ukarabati wa Uwanja wa Kumbumbu ya Sokoine lengo likiwa ni kuuweka kweny hadhi stahiki ya kutumiwa kwa mashindano mbalimbali ikiwemo Ligi kuu ya Tanzania bara.

 

Katibu wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Mkoa wa Mbeya, Langaeli Akyoo alisema kuwa maboresho yanayofanyika ni pamoja na kupaka rangi kwenye viti vya kukalia mashabiki, kufunga seng'enge mpya na kujenga vibanda vipya vya benchi la ufundi.

 

Akyoo alisema ukarabati huo ni utekelezaji wa maelekezo ya  barua waliyopokea kutoka Shirikisho la soka Tanzania (TFF) ya kuwataka wamiliki hao kufanya maboresho kadhaa katika uwanja huo ili kuendana na viwango vinavyohitajika.

 

"Tulipokea barua kutoka TFF ikitutaka, kufanya ukarabati na maboresho kadhaa, ikiwemo kupaka rangi viti vinavyokaliwa na mashabiki, kufunga seng'enge vizuri kuzunguka uwanja na kujenga upya vibanda vinavyokaliwa na benchi la ufundi, na tayari zoezi hili tunaendelea nalo" alisema Akyoo

 

Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Mbeya, Patrick Mwalunenge, akiwa ameongozana na Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (M-NEC), Ndele Jailos Mwaselela na Katibu Mwenezi Christopher Uhagile jana walifika uwanjani hapo kukagua maendeleo ya ukarabati huo unaoendelea.

 

Akiwa eneo la tukio Mwalunenge alisema kuwa wametenga zaidi ya shilingi milioni 10 ambazo zitatumika kupaka rangi kuzunguka uwanja, na kudai kuwa mpango uliopo ni kufanya ukarabati mkubwa ikiwa ni pamoja na kujenga majukwaa ya mashabiki ili wasilowe na mvua pia kujenga vibanda vya kisasa vya kufanyia biashara kuzunguka uwanja.

 

"Mpango wetu ni kuufanya uwanja wetu uvutie zaidi, kwahiyo tunaendelea kutafuta wadau mbalimbali watakao tuunga mkono ili tufanye maboresho makubwa sana kwenye uwanja wetu huu,  tutajenga majukwaa kuzunguka uwanja hata kama mvua inanyesha mashabiki wasilowe, pia tuna mpango wa kufunga taa ili mpira uchezwe hata nyakati za usiku" alisema Mwalunenge

 

Kwaupande wake Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (M-NEC), Ndele Mwaselela alimpongeza Mwenyekiti Mwalunenge kwa jitihada hizo,  kwa madai kuwa kazi hizi za kujitolea zinahitaji zaidi moyo wa kujitoa.

 

Meneja wa uwanja Modestus Mwaluka alisema rangi inayopakwa uwanjani hapo ni ya kijani na njano na kueleza kuwa mkandarasi aliyepewa kazi hiyo anatarajia kukamilisha kazi hiyo ndani ya siku saba.

No comments:

Post a Comment